Home Simba SC TABASAMU LA JOHN BOCCO LIWASHTUE WALIONUNA

TABASAMU LA JOHN BOCCO LIWASHTUE WALIONUNA


KUNA watu ambao asili yao ni kununa katika kila jambo liwe zuri hata baya yeye ataamua kununa ilimradi  ni tabia yake na ni maisha yake ambayo ameyachagua.

 Katika hilo huwezi kumuamulia mtu aina ya maisha kwa sababu ni jambo ambalo amelichagua kulifanyia kazi.

Kazi hiyo ni yake na huwezi kumzuia kwa kuwa asili hudumu na kubadili itachukua muda lakini acha iwe hivyo ni muhimu kuona maisha yanaendelea.

Lipo jina la  mzawa ambaye ni mshambuliaji John Bocco uwezo wake ni mkubwa na wachache wanatambua kazi yake huku wengine wakimbeza pia katika hilo acha iwe hivyo.

Bocco asili yake imekuwa ni kutabasamu hata anapopitia magumu hii ni asili yake kwa muda mrefu anapokuwa uwanjani ila wapo ambao wananuna juu ya uwezo wake hivyo inapaswa liwashtue wale ambao wananua juu yake.

Weka kando uwezo wake wa kufunga na kuongoza akiwa ni nahodha, bado kuna tatizo la ushambuliaji kwa wazawa jambo hilo inapaswa litazamwe kwa ukaribu na wale wengine na pia ni muhimu kwa wazawa kufikiria mara mbili namna watakavyoweza kurithi mikoba yake pale atakapojiweka kando na soka.

Tatizo la ufungaji kwa Tanzania limekuwa ni wimbo wa taifa wakati huu jambo ambalo linapaswa kutatuliwa na washambuliaji wazawa ili kuwa bora pale wanapokuwa katika majukumu ya timu ya Taifa.

Ikiwa kila mmoja atapambana ili naye aweze kutabasamu kama Bocco itafanya taifa kuwa na wachezaji wengi katika kikosi cha timu ya taifa na kufanya mashabiki kuendelea kufurahia matunda ya nyota wao.


 Tabia ya kununa pale wengine wanapofanya vizuri haiwezi kuleta matokeo kwani hili tatizo la ubutu wa washambuliaji ni kubwa na linazidi kukua kila iitwapo leo.

Mara nyingi Bocco amekuwa akiachia tabasamu pale anapofunga ama timu yake inapofunga hii ni alama ambayo inaishi na hata akiondoka kesho katika mpira tabasamu lake litaishi.

Licha ya kwamba amecheza muda mfupi ndani ya ligi ameweza kutupia mabao 13 akiwa ni namba moja kwa wazawa hivyo tabasamu lake linapaswa kuwahukumu wale ambao wamenuna.

SOMA NA HII  KUHUSU KUCHEZA NNJE YA NCHI...MANULA AVUNJA UKIMYA...ATAJA CHANGAMOTO ANAYOPITIA...

Tabasamu la Bocco linaonekana huku akiwa ni mchezaji asiyekuwa na uhakika wa kuanza kikosi cha kwanza katika mechi zake ambazo anacheza. 


Hii inatokana na kusumbuliwa na majeraha ya mara kwa mara ila kila anapopewa nafasi anafunga na kutengeneza nafasi za mabao.


Basi kwa kuwa timu ya taifa ya Tanzania inahitaji zaidi tabasamu ni muhimu wengine kujifunza kutoka kwa Bocco pamoja na washambuliaji wengine kupata matoke chanya.

Idadi ya wazawa ambao ni washambuliaji asilia tabasamu kwao ni jambo gumu kupatikana na hii inatokana na mazingira ambayo wapo pamoja na mambo mengine ambayo wanayajua wenyewe.


Wageni wamekuwa wakifanya vizuri katika suala la ufungaji hasa wanapopata nafasi ya kucheza hapa Bongo. Ufalme wa kiatu cha ufungaji kwa muda wa miaka miwili mfululizo umekuwa miguuni mwa raia wa Rwanda, Meddie Kagere ambaye yupo Simba.

Pia kwa sasa kinara wa mabao ni Prince Dube raia wa Zimbabwe yupo zake Azam FC hivyo jambo la msingi ni kuona kwamba tabasamu la Bocco linaishi kwa wazawa na kila mmoja atimize yale ambayo yanamuhusu.

Kila kitu kinawezekana na kila mshambuliaji ana uwezo wa kuonyesha tabasamu akiamua. Hivyo ni wakati wa wazawa kushtuka na kurudisha tabasamu katika kucheka na nyavu.


Wale ambao wananuna pale ambapo wazawa wanafanya vizuri basi hakuna namna ni lazima wakubali kwamba wanapokuwa wananuna wawe na sababu, kila la kheri wazawa katika utendaji  wa majukumu yenu.